Watu wawili wameuawa na wengine 60 kujeruhiwa kufuatia milipuko
miwili katika mji mkuu wa Kenya Nairobi ambayo imelenga mabasi mawili ya
abiria.
Mabasi hayo yalilipuliwa katika eneo la barabara ya Thika karibu na mji mkuu.

Mlipuko mmoja umetoa katika basi la abiria ambalo lilikua likisafirisha
abiria kutoka mjini Nairobi katika barabara ya Thika ambayo kawaida ina
shughuli nyingi.
Basi la pili lililipuliwa karibu na hoteli moja iliyo umbali wa
dakika chache kutoka jengo kubwa zaidi la maduka katika katika eneo
hilo.
Shughuli za uokoaji zinaendelea na bado hakuna taarifa rasmi
kuhusiana na watu waliouawa au kujeruhiwa kwa jumla. Picha za
televisheni zinaonyesha mabasi hayo yakiwa yameharibiwa na madirisha
kuvunjika.
Ni hapo jana tu ambapo watu wanne waliuawa na wengine wapatao
ishirini kujeruhiwa katika shambulio lingine ambapo grunedi ilirushwa
katika kituo cha mabasi ya abiria.
Shambulio la pili lilitokea karibu na mkahawa mmoja maarufu lakini hakuna mtu aliyejeruhiwa.
Mashambulio haya yanatokea mwezi mmoja tu baada ya serikali kuanzisha
oparesheni ya usalama baada ya kukumbwa na mashambulio mengine hapo
awali na pia kupata vitisho kutoka kwa kundi la wanamgambo wa Alshabab
waliodai kutekeleza shambulio la Westgate ambapo zaidi ya watu sitini
waliuawa.